MRADI wa Kituo cha Kupooza na Kusambaza Umeme toka Makambako mkoani Njombe hadi Songea mkoani Ruvuma ambao umegharimu shilingi bilioni 216 umekamilika kwa asilimia 100 .
Waziri wa Nishati Dkt.Merdad Kelamani amesema utekelezaji wa mradi huu ulianza Septemba 2016 na kukamilika Septemba 2018 na kwamba mradi huo ni miongoni mwa miradi mikubwa inayotekelezwa na Serikali kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi
Dkt.Kelamani amesema sehemu ya kwanza ya mradi huu imehusisha ujenzi wa vituo vitatu vya kufua umeme mkubwa wa kilowatts 220 vilivyojengwa Makambako, Madaba na Songea na kwamba Sehemu ya pili ya mradi imehusisha ujenzi wa miundombinu ya kusafirishia umeme unaofuliwa katika vituo hivyo vitatu
“Sehemu ya tatu ya mradi ni kusambaza umeme katika vijiji 122 vya mikoa miwili ya Njombe na Ruvuma,Mradi wa Umeme Makambako-Songea utaunganisha wateja wa awali wapatao 22,700 na kadri unavyoendelea wananchi wengi zaidi wataendelea kuunganishwa’’,anasisitiza Dkt.Kalemani.
Amesema mradi huo ambao umegharimu shilingi bilioni 216 ambazo zimetolewa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na Serikali ya Swedeni na mradi huu unatarajiwa utafunguliwa rasmi mwisho wa mwezi huu wa Septemba
Hata hivyo amesema Ifikapo Septemba 26 mwaka huu itawashwa mitambo na wananchi wataanza rasmi kutumia umeme kutoka kwenye mradi huu wa Makambako-Songea
Amesema mradi huu utakuwa na manufaa makubwa ikiwemo wananchi kuunganishiwa umeme kwa bei nafuu ya mradi wa REA ya shilingi elfu 27
“Tukiwasha mitambo ya mradi huu tutazima rasmi mitambo ya umeme iliyokuwa inatumia mafuta mazito iliyoko Madaba, Ludewa, Mbinga, Namtumbo na Songea Mjini’’,anasisitiza Waziri wa Nishati.
Amesema Mitambo ya umeme inayotumia mafuta mazito ilikuwa inagharimu shilingi bilioni 1.9 kwa mwaka.Ametoa wito kwa wananchi watumie umeme huu mkubwa kwa ajili ya kujenga uchumi wa viwanda
Kulingana na Dkt.Kalemani hadi sasa kuna jumla ya Megawatts 1568 kwenye gridi ya taifa na kwamba matarajio ni kuunganisha umeme kwenye vijiji 5100 nchini ambapo kuanzia Julai hadi Septemba 2018 tayari vijiji 818 vimeshaunganishwa
“Ifikapo Juni 2021 vijiji vyote 12,268 vya Tanzania vitakuwa vimeunganishiwa umeme,Mradi wa kuzalisha megawatts 600 za umeme wa makaa ya mawe utaanza Julai 2019,Kuanzia tarehe 15 Septemba 2018 tumetangaza kuwa wawekezaji wenye nia na uwezo wa kuzalisha umeme wa upepo na jua waje kuanza uzalishaji’’,anasema.
Hata hivyo amesema Miaka miwili ijayo serikali inatarajia kuanza kuzalisha megawatts 30 za umeme wa jotoardhi ambapo mradi wa Kinyerezi umekamilika kwa asilimia 100, na kwamba hadi sasa imeingiza megawatts 218 kwenye grid ya taifa na kufikia mwisho wa mwezi Septemba megawatts zote zitakuwa zimeingia.
*Imeandaliwa na Idara ya Habari-MAELEZO*
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa