Chama cha Mapinduzi (CCM) kimezindua rasmi kampeni zake za kumnadi mgombea wake wa ubunge katika Jimbo la Songea Mjini, Dkt. Damas Ndumbaro, kupitia mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika tarehe 14 Septemba 2025 katika viwanja vya Shule ya Msingi Kiblang'oma.Uzinduzi huo ulihudhuriwa na maelfu ya wanachama na wapenzi wa CCM, ambapo lengo kuu lilikuwa ni kumnadi Dkt. Ndumbaro pamoja na wagombea wa nafasi za udiwani kutoka kata zote za Jimbo la Songea Mjini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Songea Mjini, Ndugu Mwinyi Msolome, aliwashukuru wanachama kwa kujitokeza kwa wingi na kuonyesha mshikamano wa hali ya juu. Aidha, aliwataka wananchi wa Songea Mjini kujitokeza kwa wingi ifikapo Oktoba 29, 2025 ili kumpigia kura Dkt. Damas Ndumbaro kama Mbunge pamoja na madiwani wote wa CCM katika kata zao.
Kwa upande wake, Dkt. Ndumbaro aliwashukuru wanachama na wananchi kwa imani waliyoionyesha kwake, huku akiainisha vipaumbele vya Ilani ya CCM ambavyo ataendelea kuvisimamia iwapo atapewa ridhaa tena kuwaongoza. Mambo aliyoyataja ni pamoja na:
Kuendeleza utoaji wa ruzuku ya mbolea kwa wakulima, Ujenzi na uboreshaji wa shule za msingi na sekondari, Ujenzi wa chuo cha elimu ya juu katika jimbo, Utoaji wa pembejeo za kilimo kwa wakati, Ujenzi wa masoko ya kisasa, Uboreshaji wa uwanja wa ndege wa Songea, Kuinua sekta ya michezo kwa vijana wa jimbo hilo
Katika hatua nyingine, Mgombea Ubunge wa Jimbo la Ikungi Magharibi, Mhe. Elibariki Kungi, ambaye pia alihudhuria mkutano huo, aliwaomba wananchi wa Songea Mjini kumchagua Dkt. Ndumbaro kwa mara nyingine akisema kuwa amekuwa kiongozi mwenye utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020, na ameleta maendeleo makubwa katika kipindi chake cha uongozi.
Mhe. Elibariki aliwasihi pia wananchi hao kumpigia kura Mgombea Urais wa CCM Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mgombea Mwenza Dkt. Emanuel Nchimbi katika Uchaguzi Mkuu ujao.
MWISHO
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa