MKUU wa wilaya ya Nyasa Isabela Chilumba akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma amekagua Msitu wa Hifadhi ya asili ya Chiwindi yenye ukubwa wa hekta 3000 iliyopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.
Uchunguzi umebaini kuwa kuna uchafuzi wa kutisha katika Mto Chiwindi unaopita ndani ya hifadhi hiyo.Mto huo ambao unatumiwa na nchi zote mbili upo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.
Mto huo unamwaga maji yake ziwa Nyasa ni mchafu mwaka mzima kutokana na kuchafuliwa na wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu toka nchi zote mbili ambao wanatumia kemikali ya zebaki kusafishia dhahabu.
Uchunguzi uliofanya na Bonde la Maji la ziwa Nyasa unaonesha kuwa kati ya mito mikubwa minane inayoingiza maji katika ziwa Nyasa,mto Chiwindi unaoongoza kwa uchafuzi wa taka za zenye sumu ambazo zinaleta athari kubwa kwa viumbehai wa mtoni na ziwa Nyasa.
Mkuu wa wilaya na ujumbe wake walivuka mpaka wa Tanzania na kuingia nchini Msumbiji katika wilaya ya Kobwe Jimbo la Niassa na kuzungumza na wananchi hao juu ya umuhimu wa kuwaelimisha wananchi wa pande zote mbili kuacha kutumia kemikali zenye sumu katika mto Chiwindi na kuhifadhi msitu wa Chiwindi ambao nchini Msumbiji unaitwa Shiwindi.
Chilumba amewaeleza wananchi wa Msumbiji kuwa Agosti mwaka huu ulifanyika mkutano wa ujirani mwema baina ya Tanzania na Msumbiji katika hoteli ya Hunt Club ya Songea mkoani Ruvuma.
Mkutano huo ulishirikisha watendaji na wakuu wa wilaya za mikoa ya Mtwara na Ruvuma na wakuu wa wilaya na magavana wa majimbo ya CaboDelgado na Niassa toka nchini Msumbiji.Mkutano huo pia uliwashirikisha balozi wa Msumbiji nchini Tanzania na balozi wa Tanzania nchini Msumbiji.
Mkutano ulipitisha maazimio 12 ambayo yanahitaji utekelezaji ambao utatoa matokeo makubwa.Moja ya maazimio hayo ni kuongeza jitihada za kulinda mazingira katika Bonde la ziwa Nyasa nchini Tanzania na Bonde la Niassa nchini Msumbiji kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa