Na; Amina Pilly.
\Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Kapenjama Ndile, amempongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea, Wakili Muhoja, kwa hatua ya kizalendo ya kutenga bajeti kwa ajili ya ushiriki wa watumishi wa halmashauri hiyo katika mashindano ya SHIMISEMITA, yanayotarajiwa kuanza kitaifa tarehe 15 Agosti, 2025 jijini Tanga.


Akizungumza katika kikao maalum na wanamichezo hao, Mhe. Ndile alisema kuwa ushiriki wa watumishi katika michezo hiyo ni utekelezaji wa sera ya taifa na agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, linalozitaka Wizara, Taasisi, na Idara za Serikali kuhakikisha wanakuwa na mashirikisho ya michezo yanayojumuisha watumishi wa umma.
Ameeleza kuwa Mkoa wa Ruvuma, kupitia mji wa Songea, una historia kubwa ya michezo ambayo chimbuko lake liliasisiwa na hayati Dkt. Lawrence Gama, aliyewahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma na mpenda michezo hodari.
"Mji wa Songea ni nyumbani kwa timu ya Majimaji na Uwanja wa Majimaji, uliowekwa msingi kupitia juhudi za wanamichezo wa wakati huo. Historia hii ni ya kipekee, na tunayo dhamana ya kuendeleza urithi huu," alisema DC Ndile.
Aliwataka wanamichezo hao kuonesha nidhamu, ustaarabu na bidii uwanjani huku wakilenga ushindi, akiahidi kutoa zawadi nono iwapo timu hiyo itarejea na ngao ya ushindi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea, Wakili Muhoja, alisema kuwa kwa mwaka wa fedha 2025/2026, halmashauri imetenga bajeti ya shilingi milioni 61 kwa ajili ya kugharamia ushiriki wa watumishi katika michezo hiyo. Bajeti hiyo inahusisha gharama za usafiri, posho, vifaa vya michezo na ada ya ushiriki.

Miongoni mwa michezo ambayo watumishi wa halmashauri hiyo watashiriki ni pamoja na mpira wa miguu, mpira wa pete, mpira wa wavu, kuvuta kamba, drafti, na bao. Aidha, ameahidi kuwa katika bajeti ya mwaka 2026/2027, halmashauri itapanua wigo wa ushiriki kwa kujumuisha michezo mingine kama kwaya.
Nahodha wa timu hiyo, kwa niaba ya wanamichezo wote, alitoa shukrani kwa Mkurugenzi, Menejimenti ya Halmashauri, pamoja na viongozi wa Wilaya na Mkoa kwa kuwawezesha kushiriki michezo hiyo, huku akiahidi kuwa timu yao itacheza kwa nidhamu, uadilifu na kurudi na ushindi wa kishindo
Tukio limefanyika leo tarehe 13 Agosti 2025 katika viunga vya ofisi ya Halmashauri ya Manispaa ya Songea ambalo lilishirikisha wanamichezo hao, wakuu wa Idara na Vitengo pamoja na watumishi wa Halmashauri hiyo.
Mwisho.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa