Na, Amina Pilly
Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mheshimiwa Wilman Kapenjama Ndile, amezindua rasmi Dawati la Huduma za Ustawi wa Jamii katika Stendi Kuu ya Mabasi, kata ya Shule ya Tanga, Halmashauri ya Manispaa ya Songea, Juni 23, 2025.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Ndile amesema kuwa Serikali imeanzisha mradi huu kwa lengo la kukomesha tatizo la watoto kuzagaa kwenye maeneo ya stendi na masoko huku akisisitiza kuwa badala ya kuwaacha walale kwenye mitaro na magofu, watoto hao watasafirishwa na kurejeshwa kwenye familia zao.
Hata hivyo, Mhe. Ndile ametoa wito kwa wanasongea kutoa taarifa kwa Maafisa Ustawi pale wanapoona watoto wakizagaa katika maeneo hayo na kukomesha tatizo la watoto kulandalanda.
“Kwa wale wanao ruhusu watoto wazurure, kuuza mifuko (vifungashio) badala ya kusoma watachukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kupelekwa Mahakamani” Alisema Mhe. Ndile.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Manispaa ya Songea, Amosi Mwenda, amesema lengo la kufungua dawati hilo katika Stendi ya Tanga ni kuwapata watoto walio chini ya miaka 18 ili kuweza kuwaunganisha na familia zao hususani waliopotea na waishio kwenye mazingira magumu ambao wamekosa malezi.
Mwenda ameongeza kwa kusema dawati hilo limewekwa katika maeneo ya stendi kwa sababu kuna baadhi ya watoto wengine husafiri kutoka mikoa mbalimbali na wanapatikana katika maeneo hayo.
Aidha, Subira Mshana, amebainisha kuwa kuanzishwa kwa Dawati la Ustawi wa Jamii siyo tu utekelezaji wa mwongozo wa kimataifa kuhusu huduma hizo katika vituo vya usafiri, bali pia ni hatua madhubuti ya kuhakikisha kila mtoto anapata huduma muhimu kwa wakati.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa