WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Seleman Said Jafo ameziagiza Halmashauri zote nchini kutangaza katika vyombo vya habari miradi yote inayotekelezwa na TAMISEMI ili wananchi wafahamu.Waziri Jafo ametoa agizo hilo Jijini Mwanza wakati anazungumza na Timu za watalaam wa Halmashauri nchini ambazo zinatekeleza mradi wa program ya uboreshaji wa Miji na Manispaa (ULGSP).
Amesema TAMISEMI inatekeleza miradi mingi ikiwemo ujenzi wa barabara za Halmashauri na miradi mingine ambayo inatekelezwa lakini kutokana na kutotangazwa haifahamiki kwa wananchi ambao wanatakiwa kufahamu utekelezaji wa miradi hiyo.Hata hivyo amesema utekelezaji wa Mradi wa ULGSP umeongezewa muda kwa miezi 18 ambapo sasa utakamilika Juni 30 2020.
Kikao hicho ambacho kilifanyika kuanzia Oktoba 23 hadi 26,kiliandaliwa na Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Benki ya Dunia ambapo Halmashauri 18 nchini zinatekeleza mradi wa ULGSP.Lengo la kikao hicho lilikuwa ni kujadili maendeleo ya mradi na kufanya ufuatiliaji wa pamoja wa miradi kwa kuangalia mifano ya Halmashauri zilizotekeleza miradi vizuri na Halmashauri ambazo hazikufanya vizuri.
Zaidi ya sh.bilioni 14 zinatarajiwa kutumika katika wa ujenzi wa barabara za mji wa Songea katika kiwango cha lami zenye urefu wa kilometa 8.6.Fedha za mradi huo zimetolewa na Benki ya Dunia chini ya Mpango wa kuzijengea uwezo serikali za mitaa(ULGSP), mpango huo unakusudia kuendeleza miundombinu ya Halmashauri za miji na manispaa 18 za Tanzania Bara ikiwemo Manispaa ya Songea.
Imetolewa na Albano Midelo
Afisa Habari Manispaa ya Songea
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa