MWANACHAMA aliyejisajiri katika Mfuko wa Afya ya Jamii(CHF) kupitia CHF iliyoboreshwa anaweza kupata huduma za afya katika vituo vyote ndani ya mkoa.
Serikali imeamua kuboresha Mfuko wa Afya ya Jamii(CHF) kutoka kutoa huduma katika Kituo walichojiandikishia na sasa kupata huduma za afya katika vituo vya huduma za afya vilivyopo ndani ya mkoa.
Akizungumza katika mafunzo ya siku tatu kwa washiriki 83 wa mafunzo ya CHF iliyoboreshwa toka vituo 20 vya Halmashauri ya Manispaa ya Songea,Mwezeshaji wa Mafunzo hayo Anton Mhina amesema CHF iliyoboreshwa itamwezesha mwanachama kupata huduma ya afya kwenye kituo chake,hospitali za wilaya na mkoa.
Hata hivyo amesema ili kuhakikisha huduma zinapatikana kwa uhakika katika vituo vyote,mwanachama wa CHF hivi sasa atalipia kwa mwaka shilingi 30,000 badala ya 10,000 na kwamba serikali itachangia shilingi 30,000 hivyo kufanya kwa mwaka mzima CHF iliyoboreshwa kila kaya kuchangiwa jumla ya shilingi 60,000.
“Katika CHF iliyoboreshwa kila kaya itasajiri watu sita wakiwemo wategemezi watano na Mkuu wa Kaya,kila mtegemezi atapewa kadi yake ya afya badala ya kadi moja kutumiwa na wote,baada ya kujisajiri haizidi siku mbili Mwanachama anakuwa amepata kadi yake’’,anasisitiza Mhina.
Kwa upande wake Kaimu Mganga Mkuu wa Manispaa ya Songea Dk.Mameritha Basike amewataja washiriki wa mafunzo hayo toka Manispaa ya Songea kuwa ni wenyeviti wa kamati za afya za mitaa,wauguzi wa vituo vya afya,wahasibu na wawezeshaji wanane kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na TAMISEMI.
Ameyataja mafunzo ambayo yametolewa kwa washiriki hao kuwa ni CHF iliyoboreshwa,mafunzo ya utoaji wa fedha kwenye vituo na manunuzi ya dawa kupitia ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma.
Akizungumza wakati anafungua rasmi mafunzo hayo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea Tina Sekambo ametoa rai kwa washiriki kufuatilia kwa makini mafunzo hayo ili kutoa habari sahihi kwa wananchi kuhusu manufaa ya CHF iliyoboreshwa.
CHF iliyoboreshwa ni Bima ya Afya kwa ajili ya wananchi wa ambao hawana uwezo au hawajatimiza vigezo vya kujiunga na Bima ya Afya ya Taifa (NHIF).
CHF iliyoboreshwa imeanzishwa kuondoa changamoto zilizokuwepo kwenye mfuko wa afya ya jamii (CHF) ulioanzishwa mwaka 2001.
Imeandaliwa na Albano Midelo
Afisa Habari Manispaa ya Songea
Mei 8,2018
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa