Kamati ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Ruvuma, ikiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Ruvuma, Komredi Oddo Mwisho, imefanya ziara ya kukagua na kutathmini utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika kata tofauti ndani ya Manispaa ya Songea, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa CCM.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Komredi Oddo Mwisho amewataka wataalamu ngazi zote kuendelea kuboresha utendaji wao wa kazi hususan katika usimamizi wa miradi ya maendeleo, ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa. Ameelekeza pia kukamilishwa kwa majengo ambayo bado hayajakamilika ili kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani.
Aidha, Komredi Oddo Mwisho amesema baadhi ya changamoto zilizopo zinaweza kutatuliwa katika ngazi za kata au mitaa bila kusubiri hatua za juu, na kupitia changamoto ya majengo ambayo hayajakamilika, amemtaka Mkurugenzi wa Manispaa kuhakikisha yanakamilishwa kwa haraka. Vilevile amesisitiza upakaji rangi kwenye majengo yaliyochakaa ili kuboresha miundombinu na mandhari ya maeneo ya utoaji huduma za kijamii.
Miongoni mwa miradi iliyotembelewa katika ziara hiyo ni ujenzi wa Shule Mpya ya Elimu ya Msingi AMALI, ujenzi wa madarasa mawili katika Shule ya Msingi Amani, pamoja na mradi wa FAST TRACK uliopo katika Kituo cha Afya Mjimwema.
Ziara hiyo imefanyika leo, tarehe 02 Februari 2026, na imehudhuriwa na viongozi wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, wataalamu wa ngazi ya Mkoa pamoja na wataalamu kutoka Manispaa ya Songea
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa