Songea, Ruvuma – Juni 2, 2025:
Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Ndugu Emmanuel John Nchimbi, ameongoza mamia ya waombolezaji katika mazishi ya Muasisi wa Chama cha TANU na mpigania uhuru wa Tanganyika, Hayati Alhaji Mustafa Mohammed Songambele, yaliyofanyika katika Kijiji cha Bombambili, Wilaya ya Songea, Mkoa wa Ruvuma.
Hayati Songambele alifariki dunia tarehe 1 Juni 2025 akiwa na umri wa miaka 100, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili. Marehemu alizaliwa tarehe 25 Mei 1925 na aliadhimisha karne moja ya maisha yake tarehe 25 Mei 2025.
Katika hotuba yake, Katibu Mkuu Nchimbi alisema:
“Chama cha Mapinduzi na Serikali vimepata msiba mkubwa. Tumempoteza mmoja wa waasisi mashuhuri wa TANU, mzalendo na shujaa wa uhuru wa taifa letu. Mzee Songambele ametuachia hazina kubwa ya historia ya nchi kupitia kitabu alichoandaa kiitwacho Safari ya Karne. Chama kitadhamini na kusimamia kukamilika kwa kitabu hiki ili Watanzania wapate kujifunza kutoka maisha yake.”
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mhe. Kanali Ahmed Abbas Ahmed, aliwasilisha salamu za pole kwa familia ya marehemu na kusema:
“Tumempoteza kiongozi mwenye busara, aliyekuwa tayari siku zote kutoa ushauri na hekima kwa vizazi vya sasa. Ni jukumu letu kuendeleza misingi ya haki, utu na uzalendo aliyoisimamia.”
Wasifu wa marehemu ulisomwa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Namtumbo, ambapo ilielezwa kuwa Hayati Songambele alikuwa Mkuu wa Wilaya ya kwanza wa Ilala baada ya uhuru mwaka 1961, na pia alihudumu kama Mkuu wa Mikoa ya Pwani (sasa Dar es Salaam) na Shinyanga. Pamoja na kuwa muasisi wa TANU, alikuwa miongoni mwa waanzilishi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA).
Hayati Songambele ameacha wake watatu, watoto 27 na wajukuu 74. Amezikwa kijijini kwao Bombambili kwa heshima za kitaifa na kwa uwepo wa viongozi mbalimbali wa serikali, chama na wananchi wa Ruvuma.
Mwisho
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa