Na; AMINA PILLY
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Songea, Mheshimiwa Michael Mbano, leo tarehe 16 Juni 2025, ameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika katika Kata ya Mfaranyaki, Halmashauri ya Manispaa ya Songea.
Katika hotuba yake, Mhe. Mbano amesema kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira bora kwa watoto kwa kutoa elimu bure kuanzia ngazi ya shule ya msingi hadi kidato cha sita, pamoja na kuboresha upatikanaji wa chanjo na huduma bora za afya. Aidha, amesema serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kupambana na ndoa za utotoni na ajira za watoto.
Hata hivyo, Meya Mbano ametaja kuwepo kwa changamoto zinazowakumba watoto, hasa wale wa mitaani ambao hukosa fursa ya kupata elimu kutokana na umasikini na kukumbwa na vitendo vya ukatili wa kijinsia.
“Serikali ina wajibu wa kuhakikisha kuwa mustakabali wa mtoto wa Afrika ni wenye tumaini. Hii inahitaji kuwekeza zaidi katika elimu bora na jumuishi, huduma za afya kwa watoto hususani vijijini, ulinzi dhidi ya ukatili wa aina zote, pamoja na ushiriki wa watoto katika maamuzi yanayowahusu,” alisema Mheshimiwa Mbano.
Aidha, ametoa wito kwa jamii, wazazi na walezi kuwalea watoto kwa maadili mema, kuwalinda, na kuwawezesha kutimiza ndoto zao.
Kwa upande wake, akisoma risala kwa niaba ya watoto mbele ya mgeni rasmi, Happiness Mbunda ameiomba Serikali pamoja na wadau wa maendeleo kuendelea kushirikiana kwa karibu ili kuimarisha ulinzi wa mtoto. Alisisitiza kuwa taifa imara hujengwa kwa kuwekeza katika maendeleo ya watoto wake.
Siku ya Mtoto wa Afrika huadhimishwa kila mwaka tarehe 16 Juni, kwa kumbukizi ya mauaji ya watoto wa Soweto nchini Afrika Kusini mwaka 1976 waliouawa walipokuwa wakipigania haki yao ya kupata elimu bora.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa