Katibu Tawala wa Wilaya ya Songea, Mtella Mwampamba, amewapongeza Maafisa Watendaji wa Kata wa Manispaa ya Songea kwa jitihada zao katika kusimamia utekelezaji wa mkataba wa lishe, hatua iliyochangia kupanda kwa utekelezaji kutoka asilimia 32 hadi asilimia 74.7 katika robo ya pili ya mwaka huku akisisitiza kuongeza juhudi ili kuongeza asilimia 2 pekee kufikia mstari wa kijani.
Mwampamba amesema kuwa mwanzoni mwa utekelezaji wa zoezi hilo kulikuwa na makaripio makali kutokana na matokeo yasiyoridhisha, lakini ongezeko hilo kubwa limepunguza ukali wa maneno kutoka kwa viongozi baada ya kuona matunda ya kazi inayofanywa.
Hayo yamejiri leo, Februari 11, 2026, katika kikao cha utekelezaji wa Mkataba wa Lishe kilichofanyika katika Ukumbi wa Manispaa ya Songea, kikihudhuriwa na Maafisa Watendaji wa Kata 21 kwa lengo la kufanya tathmini na ufuatiliaji wa utekelezaji wa mkataba huo.
Katika maelekezo yake, Mwampamba alinukuu agizo la Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan la Januari 26 mwaka huu, kuwa suala la Bima ya Afya kwa Wote liwe ajenda ya kudumu katika kila kikao. Hivyo, alielekeza kuwa kuanzia sasa, bima ya afya itakuwa ajenda ya kudumu katika vikao mbalimbali vya kamati ya maendeleo ya kata katika halmashauri hiyo.
Alisema jukumu la watendaji litakuwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu Bima ya Afya kwa Wote, pamoja na kutambua makundi yatakayonufaika, ikiwemo watu wenye ulemavu, watoto chini ya miaka mitano na wazee. Alieleza kuwa Serikali imewekeza fedha nyingi kuhakikisha huduma hiyo inatolewa kwa ufanisi, huku akiwataka watendaji kujiandaa kusimamia utekelezaji wake na kuhakikisha kila mwananchi anasajiliwa.
Aidha, alitoa taarifa kuhusu maadhimisho ya kumbukizi ya Vita vya Majimaji yanayofanyika kila mwaka Februari 27, ambapo mwaka huu mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi.
Katika hatua nyingine, halmashauri ilitoa vyeti vya pongezi kwa kata zilizofanya vizuri katika afua ya utoaji wa chakula kwa wanafunzi shuleni. Kata zilizotajwa kufanya vizuri ni Matogoro, Matarawe, Subira na Mjini, huku Kata ya Matogoro ikiongoza.
Akizungumza kwa niaba ya washindi, Afisa Mtendaji wa Kata ya Matogoro, Bi. Neema Hinju, alisema kata hiyo ina jumla ya shule tano, zikiwemo tatu za msingi na mbili za sekondari. Alibainisha kuwa mafanikio yao yametokana na ushirikiano kati ya wazazi, wanafunzi na bodi za shule. Aidha, alisema wameweka mkakati wa kila shule kuwa na robo tatu ya ekari ya zao la mahindi ili kuimarisha upatikanaji wa chakula shuleni, sambamba na michango ya wazazi
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa