MTO Ndumbi uliopo katika Kijiji cha Mkili Kata ya Nindai Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma umekuwa unasababisha majanga kwa jamii ikiwemo kusababisha vifo na ulemavu wa kudumu.
Afisa Mtendaji wa Serikali ya Kijiji hicho Nathan Kambanga amekiri mto huo ambao unamwaga maji yake ziwa Nyasa kipindi cha masika unapofurika umekuwa unasababisha athari kijamii na kiuchumi ikiwemo baadhi ya watu kupoteza maisha.
Esau Mwanja akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Kijiji hicho amedai kuwa hadi sasa tayari watu kumi wamepoteza maisha baada ya kusombwa na maji ya mto huo ambapo kuna watu kadhaa ambao wamepata ulemavu .
“Kumbukumbu zangu zinaonesha watu Zaidi ya kumi wamekufa katika mto huu na wengine kupata ulemavu,tunaomba serikali itujengee daraja ili kunusuru maisha ya watu wa mwambao mwa ziwa Nyasa’’,anasisitiza Mwanja.
Licha ya kusababisha vifo inadaiwa mto huo pia unasababisha kila mwaka kwa miezi miwili nusu ya wanafunzi katika shule ya msingi Mkili kutohudhuria masomo ipasavyo.
Mmoja wa walimu wakongwe katika shule ya msingi Mkili Mwl. John Ntanga anasema kati ya mwezi Januari,Februari na Machi kila mwaka mto huo unapofurika husababisha wanafunzi zaidi ya 600 kushindwa kufika shuleni kutokana na mto kujaa hali ambayo inachangia kuzorotesha kwa elimu.
“Mto huo ni changamoto kubwa ambayo inachangia utoro katika shule hii,wanafunzi wanaotoka upande mmoja wa mto huo wanashindwa kabisa kuvuka kwa kuwa maji yanajaa hadi juu ya daraja,mto una nguvu kubwa umewahi kusomba gari,wanafunzi hawawezi kuvuka wanakosa masomo’’,alisisitiza.
Ntanga ambaye amekuwa Mwalimu Mkuu katika shule hiyo tangu mwaka 1997 anasema daraja hilo limekuwa kero kubwa kwa kuwa licha ya kujengwa lakini limekuwa linabomoka kutokana na kasi ya maji ya mto huo na kwamba hadi sasa ufumbuzi wake bado haujapatikana.
“Wakala wa barabara TANROAD mara kadhaa wamejaribu kulijenga daraja lakini wakati wa mvua nyingi kati ya mwezi Februari na Machi daraja limekuwa linabomoka na kusombwa na maji kwa hiyo wameamua kuacha kwa sababu ni hasara labda wajenge daraja la juu’’,alisema Ntanga.
Hata hivyo baadhi ya wakazi wa kijiji hicho wanadai kuwa tatizo la daraja limekuwa ni ahadi ambayo hadi sasa haijapatiwa ufumbuzi na kuendelea kuwa kero na kwamba wanaamini serikali ya awamu ya tano itatafutia ufumbuzi wa kudumu..
Esau Mwanja anasema eneo hilo ni hatari kwa kuwa magari yanapita ndani ya mto ambapo wakati wa masika ni hatari kwa kuwa kuna gari ambalo lilisombwa na maji wakati linavuka kwenye mto huo mkubwa ambao maji yake yanakwenda kwa kasi.
Imeandaliwa na Albano Midelo
Afisa Habari Manispaa ya Songea
Mei 9,2018
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa