Na,
AMINA PILLY,
AFISA HABARI MANISPAA.
03 MACHI 2022.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM Taifa Dkt. Edmund Mndolwa amewataka wanafunzi wote Manispaa ya Songea kuwa na nidhamu pamoja na kusoma kwa bidii ili waweze kufaulu masomo yao ipasavyo na kutimiza ndoto zao.
Dkt. Mndolwa ametoa rai hiyo akiwa Ziarani Manispaa ya Songea alipotembelea miradi ya maendeleo ambayo ni fedha za Mpango wa Maendeleo kwa ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO 19 ambapo kwa Manispaa ya Songea ilipokea fedha shilingi milioni 660 kwa ajili ujenzi wa vyumba vya madarasa 26 kwa shule ya Sekondari na madarasa matatu shule ya Msingi Shikizi.
Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 03 machi 2022 katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea ambapo aliweza kutembelea mradi wa ujenzi wa kituo cha afya kinachojengwa katika kata ya Msamala ambacho kipo hatua ya lipu pamoja na mradi wa ujenzi wa madarasa katika shule ya sekondari ya Matarawe.
Aidha, akiwa Ziarani hapo, amewataka walimu wote Manispaa ya Songea kutekeleza wajibu wao vizuri ili waweze kuwasimamia wanafunzi katika masomo yao pamoja na kukagua maendeleo ya kila mwanafunzi ili kukomesha utoro na kushuka kwa ufaulu wa mitihani kwa wanafunzi.
Amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake za kusimamia na kuendeleza miradi yote iliyoanzishwa wakati wa uongozi wa Hayati John Pombe Magufuli hususani miundombinu ya umeme, maji, Afya na Elimu.
Alisema Serikali hupanga mipango ya maendeleo kwa kufuata idadi au takwimu , hivyo amewataka wananchi wote wa Manispaa ya Songea kushiriki zoezi la Sensa ya watu na makazi ambalo linatarajia kufanyika mwaka huu kwa lengo la kupata takwimu ambayo hutumika kupanga maendeleo kwa ngazi ya jamii.
Amewataka wanachama wote wa Chama Cha Mapinduzi Songea Mjini kushiriki katika uchaguzi wa kuwapata viongozi ngazi ya chama (CCM) ambao unatarajia kufanyika hivi karibuni ambapo alisema kiongozi bora ni yule anayejituma na kutetea haki za wananchi.’Alisisitiza’
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea, Christopher Ngonyani alisema kuwa ujenzi wa kituo cha afya Msamala umetengewa kiasi cha shilingi Milioni 500 ambazo ni fedha kutoka Serikali kuu pamoja na fedha zilizochangwa na wananchi shilingi Milioni 2.5 hivyo kufanya kuwa na jumla ya shilingi Milioni 502,500,000.
Alisema kuwa lengo la kujenga kituo hicho ni kutoa huduma bora na ya karibu kwa wananchi ambapo huduma mbalimbali zitatolewa ikiwemo na upasuaji, upimaji wa VVU, maabara, jengo la wagonjwa wa nje (OPD), jengo la wodi ya wazazi pamoja na utoaji huduma bora ya afya ya mama na mtoto.
Hadi hivi sasa mradi huo umetumia jumla ya shilingi Milioni 327,469,000 kwa hatua ya plaster na dali ambapo ujenzi huo bado unaendelea. ‘Ngonyani alibainisha’
Mwisho.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa