Timu ya wataalamu ngazi ya Mkoa wa Ruvuma ikiongozwa na Katibu Tawala wa Mkoa huo, Bi Mary Makondo, imefanya ziara ya kukagua miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea kuanzia tarehe 12 hadi 13 Novemba 2025.
Akizungumza na wataalamu kwenye kata na miradi mbalimbali aliyotembelea, Bi Makondo aliwapongeza kwa usimamizi bora wa miradi inayoonyesha ubora na thamani halisi ya fedha zilizotumika.
“Pongezi kwa usimamizi wa mradi wa ujenzi wa Shule ya Amali wenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.6 fedha za SEQUIP na Shilingi Milioni 38 za mapato ya ndani, ambao upo katika hatua ya asilimia 97. Mafanikio haya yametokana na uzalendo, bidii ya kazi na uadilifu,” alisema Bi Makondo.
Aidha, aliwataka wataalamu hao kukamilisha miundombinu ya nje na kuweka mikakati endelevu ya utunzaji wa miradi ili idumu kwa muda mrefu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Akizungumzia mradi wa ujenzi wa Shule ya Jumbe Idd iliyopo Kata ya Ruhuwiko, ambao unatekelezwa kwa fedha za SEQUIP kiasi cha Shilingi Bilioni 0.581 pamoja na Shilingi Milioni 100 za mapato ya ndani, Bi Makondo alisisitiza umuhimu wa kusogeza huduma bora za elimu kwa jamii. Aliwahimiza walimu na viongozi wa Serikali za Mitaa kutunza mazingira, kudhibiti utoro wa wanafunzi, na kuendelea kushirikiana na wazazi katika uchangiaji wa chakula shuleni.
Kuhusu mradi wa maegesho ya magari makubwa (maroli), Bi Makondo aliwapongeza wataalamu kwa ubunifu na usimamizi bora wa mradi huo, akieleza kuwa ni fursa muhimu kutokana na eneo hilo kuunganisha Halmashauri za Mbinga, Songea DC na Mbinga Mji. Aliwataka wananchi na viongozi wa kata husika kulinda na kutunza miundombinu hiyo kwa matumizi ya sasa na vizazi vijavyo
Ziara hiyo imehitimishwa tarehe 13 Novemba 2025.
IMEANDALIWA NA;
AMINA PILLY,
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa