Songea, 04 Agosti 2025 – Washiriki 42 kutoka kata 21 za Halmashauri ya Manispaa ya Songea wameanza mafunzo ya usimamizi wa uchaguzi ngazi ya kata, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2025. Mafunzo hayo yanafanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Songea kuanzia leo tarehe 04 Agosti hadi tarehe 06 Agosti 2025.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Songea Mjini, Bw. Hossein Mghewa, aliwahimiza washiriki kuzingatia umuhimu wa dhamana waliyopewa.
Alieleza kuwa jukumu la kusimamia na kuratibu uendeshaji wa uchaguzi wa Rais, Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Madiwani kwa upande wa Tanzania Bara ni kubwa na lenye uzito kwa mustakabali wa taifa.
"Dhamana mliyopewa ni muhimu sana. Ni vyema mkazingatia masharti ya Ibara ya 74(6) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, inayotambua Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kuwa na jukumu la kusimamia na kuratibu chaguzi hizi muhimu kwa nchi yetu," alisema Bw. Mghewa.
Aidha, mafunzo hayo yameambatana na zoezi la kula kiapo cha kutunza siri kilichotolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Songea Mjini, Mheshimiwa Happiness Shilembi.
Akizungumza na washiriki, Hakimu Shilembi aliwasisitiza kufanya kazi kwa weledi, kufuata maelekezo yote waliyopewa katika kipindi chote cha mafunzo, na kuhakikisha wanazingatia maadili ya kazi hiyo.
Mafunzo haya ya siku tatu yanalenga kuwajengea uwezo wasimamizi hao wa kata katika maandalizi na uendeshaji wa uchaguzi ili kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa haki, amani na uwazi.
Mwisho
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa