Na;
AMINA PILLY;
AFISA HABARI SONGEA MANISPAA
02 MACHI 2022.
Halmashauri ya Manispaa ya Songea imefanya uzinduzi wa maadhimisho ya Siku ya Mwanamke Duniani kuelekea kilele cha maadhimisho tarehe 08 machi 2022 ambayo hufanyika kila mwaka Duniani kote.
Uzinduzi wa maadhimisho hayo Kihalmashauri ya Manispaa ya Songea yamefanyika katika viwanja vya bustani ya Manispaa ya Songea hapo jana tarehe 01 machi 2022 kwa lengo la kuelimisha jamii kuhusiana na usawa wa kijinsia katika nyanja za maendeleo.
Akizungumza katika maadhimisho hayo, mgeni rasmi ambaye alikuwa Kamishina Msaidizi wa jeshi la polisi Mkoa wa Ruvuma ACP Pilly Mande alitoa pongezi kwa wanawake wote wa nchi za Afrika pamoja na kuitaka Serikali kuchukua hatua katika kuhamasisha usawa katika nyanja za elimu, siasa na uchumi kwa kizazi kilichopo na kijacho ili kuleta maendeleo yenye uwiano sawa kwa wanawake na wanaume.
Mande amewataka wanawake wote nchini kutambua nafasi zao katika jamii kama walimu, wazalishaji, madaktari pamoja na walezi ili kutengeneza kizazi kinachojali utu na uzalendo kuanzia katika ngazi ya familia hadi Taifa kwa ujumla.
Amekemea suala la unyanyasaji wa kijinsia katika jamii kwa wanawake ikiwemo na kukosa haki ya kupata elimu, ubakaji pamoja na kupata mimba za utotoni na kutoa wito kwa jamii kuwa walinzi hasa kwa watoto wa kike pamoja na Taasisi za kidini kwa kuendelea kutoa elimu kwa jamii ili kuondokana na unyanyasaji wa kijinsia.’Alisisitiza’
Kwa upande wake Mratibu wa maadhimisho hayo ambaye pia ni Afisa maendeleo ya jamii Manispaa ya Songea Joyce Mwanja alisema kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kutoa fursa ya kuelimisha jamii kuhusiana na jitihada zinazifanywa na Serikali, asasi za kiraia, sekta binafsi na wadau mbalimbali katika kukuza hali ya wanawake wa kitanzania katika nyanja za maendeleo.
Katika utekelezaji wa kutatua changamoto zinazowakabili wanawake kiuchumi, Halmashauri ya Manispaa ya Songea imeendelea kuwawezesha wanawake kwa kutoa mikopo (10%) kila mwaka na katika kipindi cha mwaka 2020/2021 vikundi 1,150 vilipatiwa mikopo yenye jumla ya Tsh. 216,229,441 ambapo vikundi 957 vya wanawake vilipatiwa kiasi cha Tsh. 129,727,777, vikundi 168 vya vijana walipokea Tsh. 64,267,777 pamoja na vikundi 5 vya watu wenye mahitaji maalumu Tsh.22,233,886.”Mwanja alibainisha”
Aliongeza kuwa katika kipindi cha mwaka 2021/2022 Manispaa ya Songea kupitia mfuko wa maendeleo wa wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalumu ilitoa jumla ya Tsh. 465,000,000 ambapo vikundi 5 vya wanawake walipokea Tsh. 310,000,000, vikundi 4 vya vijana Tsh.145,000,000 pamoja na kikundi 1 cha watu wenye mahitaji maalumu Tsh. 10,000,000.
Ametoa rai kwa Serikali kuendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa wanawake ili kuwajengea ufahamu, uwezo na uzoefu ambao utawawezesha katika kurithisha vizazi vyenye haki na usawa katika ngazi zote za maendeleo.
Ikumbukwe kuwa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani ilianza kuadhimishwa rasmi duniani tarehe 8 Machi 1975 baada ya umoja wa Mataifa kuridhia siku hii kutumika kama siku rasmi kuikumbusha dunia juu ya haki za wanawake.
Kauli mbiu katika Maadhimisho haya mwaka huu ni “KIZAZI CHA USAWA KWA MAENDELEO ENDELEVU”
Mwisho.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa