TANZANIA ni miongoni mwa nchi chache duniani ambayo ina fursa za kipekee ambazo zinaweza kuchochea utalii wa ikolojia kupitia ziwa Tanganyika na ziwa Nyasa.Maziwa hayo mawili yanatajwa kuwa na aina mbalimbali za samaki wa mapambo ambao baadhi yao wana sifa ya kutoa umeme hivyo wamepewa jina la samaki umeme(electric fish).
Mhifadhi wa Hifadh za Taifa Noelia Mnyonga anawafahamu vyema samaki wanaotoa umeme waliopo katika ziwa Tanganyika na ziwa Nyasa.Mnyonga anasema samaki hao ni kivutio adimu na cha kipekee duniani na kwamba wanaweza kuwa chanzo muhimu cha mapato kwenye sekta ya utalii ambayo ni miongoni mwa sekta zinazoongoza kwa kuchangia uchumi wa Taifa.
“Samaki wanaotoa umeme wakitangazwa kikamilifu ndani na nje ya nchi watalii wengi watamiminika hapa nchini ili kufika kuwaona samaki hao wa ajabu na Taifa kupata fedha nyingi za kigeni’’,anasema Mnyonga.Anasisitiza kuwa watalii na wasomi wanaweza kufanya utafiti na kujifunza kwanini samaki hao wanatoa umeme hivyo serikali kuongeza ajira kwa kuwa vijana watapata fursa ya kuwaongoza watalii kuona kivutio hicho
Hata hivyo kwa mujibu wa mhifadhi huyo umeme unaotolewa na samaki hao ni kwa ajili ya kujilinda na maadui katika ziwa na kwamba,samaki wanapowasogelea hutoa umeme ambao hauna madhara kwa binadamu.Anasema utafiti unatakiwa kufanyika zaidi kuhusiana na samaki hao kuwa watalii na watafiti wengi wanapenda kujifunza maisha ya viumbe adimu vya nchi kavu na majini wakiwemo samaki hao wanaotoa umeme.
Bila shaka watafiti wakipata fursa ya kufika katika ziwa Tanganyika na ziwa Nyasa wangependa kufanya utafiti wa kina kufahamu idadi ya samaki hao na tabia yao ya kutoa umeme wanaposogelewa na adui.Utafiti wa awali ambao ulifanywa katika ziwa Tanganyika na Mwanasayansi Erick Fortune kutoka Chuo Kikuu cha Johns Hopkins cha nchini Marekani unaonesha kuwa samaki-umeme wana uwezo wa kutoa umeme kwa kutumia ogani umeme iliyopo kwenye mikia ya samaki hao.
Kulingana na utafiti,umeme unaotolewa na samaki umeme ni dhaifu na hauwezi kuleta madhara kwa binadamu na kwamba samaki hao wana seli nyeti juu ya ngozi zao ambazo zinawawezesha kutambua maadui na kuhisi hatari hivyo huzalisha umeme kukabiliana na maadui zao na kwamba hutumia umeme huo pia kwa mawasiliano na samaki wenzao.
Kulingana na utafiti ambao ulifanywa katika ziwa hilo na Jumuiya ya Nchi zilizo Kusini mwa Afrika(SADC) kwa kushirikiana na nchi ya Uingereza kati ya mwaka 1991 hadi 1994 na mwaka 1996 hadi 2000,ulionesha kuwa ziwa hilo lina kiasi cha tani 165,000 za samaki.Kati ya tani hizo za samaki, tani 35,000 za samaki ni jamii ya samaki wa maji ya juu ambao wanaweza kuvuliwa bila kuathiri uvuvi kila mwaka.Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nyasa Oscar Mbyuzi anasema utafiti umebaini ziwa Nyasa lina aina 503 za samaki wa mapambo ambao hawapatikani sehemu nyingine duniniani.
Mwandishi wa makala haya ni Albano Midelo
mawasiliano albano.midelo@gmail.com,simu 0784765917
Imeandikwa Julai pili,2018.
SONGEA MUNICIPAL COUNCIL
Anuani ya Posta: P O BOX 14, SONGEA
Simu ya Mezani: 025 2602970
Simu ya Kiganjani:
Barua Pepe: info@songeamc.go.tz
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Manispaa ya Songea. Haki zote zimehifadhiwa